Social Icons

Pages

Blogger templates

Friday, September 30, 2016

PATO LA TAIFA LAKUA KWA ASILIMIA 7.9



Na Beatrice Lyimo

MAELEZO

PATO la Taifa limeendelea kukua kwa asilimia 7.9 katika kipindi cha mwezi Aprili hadi Juni 2016 ikilinganishwa na kasi ya asilimia 5.8 katika kipindi kama hicho mwaka 2015.

Takwimu hizo zimetolewa leo Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa  Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Dkt. Albina Chuwa alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu hali ya pato la Taifa kwa robo ya pili  kuanzia Aprili hadi Juni mwaka 2016.

Dkt Chuwa  alisema kuwa ukuaji wa pato la Taifa umetokana na shughuli za kiuchumi ikiwemo kilimo, mifugo, misitu na uvuvi ambapo shughuli  hizo zilikuwa kwa asilimia 3.2 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 1.9 katika kipindi kama hicho mwaka 2015.

Kwa upande wa shughuli za uchumi za viwanda na ujenzi, Dkt. Chuwa alisema kumekuwa na ongezeko la asilimia 20.5 katika kipindi hicho ukilinganisha na ukuaji wa asilimia 11.2 mwaka 2015 katika shughuli za uchimbaji madini, mawe na kokoto.

Aidha katika shughuli za uzalishaji bidhaa na viwanda kumeongeza kwa asilimia 9.1 katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2016 ukilinganisha na kasi ya asilimia 5.2 ya mwaka 2015.

Katika shughuli za uchukuzi na uhifadhi, Dkt Chuwa alisema kuwa shughuli hizo zimekuwa kwa kiwango cha asilimia 30.6 zimetokana na usafirishaji wa abiria kwa njia ya reli na barabara ikiwa ni pamoja na usafiri wa UDART.

Hata hivyo katika shughuli za fedha na bima ziliongezeka kwa kasi ya asilimia 12.5 ikilinganishwa na asilimia 10.0 iliyopatikana katika kipindi kama hicho mwaka 2015.

Wakati huo huo huduma za elimu zilikuwa kwa kasi ya asilimia 8.0 katika robo hiyo ya mwaka ikilinganishwa na aslimia 7.4 ya kipindi kama hicho kwa mwaka 2015 ambapo ukuaji wa shughuli hii imetokana na ongezeko la wanafunzi waliodahiliwa mwaka 2016.

No comments:

Post a Comment