Na Jacquiline Mrisho
Benki
ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imetengewa kiasi cha shilingi
bilioni 200 katika mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya kuongeza mikopo
itakayowasaidia wakulima wadogo kuendesha shughuli za kilimo.
Hayo
yamesemwa leo mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi,
Mhe. William Ole Nashi alipokuwa akijibu swali la Mhe. Rose Sekum (Viti
Maalum) lililohoji kuhusu mpango wa Serikali kuwafikia wakulima wadogo
nchini.
Naibu
Waziri huyo amesema kuwa Serikali ilianzisha rasmi Benki hiyo mwezi
Agosti 2014 ikiwa na nia thabiti ya kuhakikisha Benki hiyo inapata mtaji
wa kutosha ili kutimiza lengo lililokusudiwa la kuwezesha upatikanaji
wa mikopo kwa wakulima wadogo.
“Serikali
itaendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya Benki hiyo ambapo kwa
mwaka huu tumetenga Shillingi Bilioni 200, hata hivyo tumejizatiti
kuongeza mtaji kupitia Hati Fungani ya mitaji isiyo ya fedha taslimu
yenye thamani ya shilingi bilioni 800”, alisema Mhe. Nashi.
Ameongeza
kuwa kufuatia ujio wa Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika
(AFDB) kumekuwa na mazungumzo baina ya benki hizo mbili juu ya kupatiwa
mkopo ambao utaiongezea mtaji Benki ya TADB ili iweze kusaidia wakulima
wengi zaidi.
Aidha,
ili kuwafikia wakulima wadogo nchini, Mhe. Ole Nashi amefafanua kuwa
Benki hiyo imejikita katika kuvijengea uwezo vikundi vya wakulima ili
viweze kukopesheka na kuwa na uwezo wa kurejesha mikopo hiyo.
Katika
utekelezaji wa mpango huo, Benki ilianza kwa kuvijengea uwezo vikundi
89 vya wakulima wadogo vyenye jumla ya wakulima 21,526 na kati ya hivyo,
jumla ya vikundi 8 vilitimiza masharti ya msingi ya kuweza kukopa na
vilikopeshwa jumla ya shilingi billion1.
Mpaka
sasa TADB inatoa huduma za mikopo kwa wakulima katika mikoa 6 kwa
kushirikiana na Sekretarieti za mikoa, Tume ya Maendeleo ya Ushirika,
Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko,
Mfuko wa Pembejeo na Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa.
No comments:
Post a Comment