Social Icons

Pages

Blogger templates

Wednesday, November 9, 2016

BENKI YA KILIMO YATENGEWA BILIONI 200 KWA AJILI YA MIKOPO KWA WAKULIMA.

 

Na Jacquiline Mrisho

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 200 katika mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya kuongeza mikopo itakayowasaidia wakulima wadogo kuendesha shughuli za kilimo.

Hayo yamesemwa leo mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mhe. William Ole Nashi alipokuwa akijibu swali la Mhe. Rose Sekum (Viti Maalum) lililohoji kuhusu mpango wa Serikali kuwafikia wakulima wadogo nchini.

Naibu Waziri huyo amesema kuwa Serikali ilianzisha rasmi Benki hiyo mwezi Agosti 2014 ikiwa na nia thabiti ya kuhakikisha Benki hiyo inapata mtaji wa kutosha ili kutimiza lengo lililokusudiwa la kuwezesha upatikanaji wa mikopo kwa wakulima wadogo.

“Serikali itaendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya Benki hiyo ambapo kwa mwaka huu tumetenga Shillingi Bilioni 200, hata hivyo tumejizatiti kuongeza mtaji kupitia Hati Fungani ya mitaji isiyo ya fedha taslimu yenye thamani ya shilingi bilioni 800”, alisema Mhe. Nashi.

Ameongeza kuwa kufuatia ujio wa Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AFDB) kumekuwa na mazungumzo baina ya benki hizo mbili juu ya kupatiwa mkopo ambao utaiongezea mtaji Benki ya TADB ili iweze kusaidia wakulima wengi zaidi.

Aidha, ili kuwafikia wakulima wadogo nchini, Mhe. Ole Nashi amefafanua kuwa Benki hiyo imejikita katika kuvijengea uwezo vikundi vya wakulima ili viweze kukopesheka na kuwa na uwezo wa kurejesha mikopo hiyo.

Katika utekelezaji wa mpango huo, Benki ilianza kwa kuvijengea uwezo vikundi 89 vya wakulima wadogo vyenye jumla ya wakulima 21,526 na kati ya hivyo, jumla ya vikundi 8 vilitimiza masharti ya msingi ya kuweza kukopa na vilikopeshwa jumla ya shilingi billion1.

Mpaka sasa TADB inatoa huduma za mikopo kwa wakulima katika mikoa 6 kwa kushirikiana na Sekretarieti za mikoa, Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, Mfuko wa Pembejeo na Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa.

MWISHO.

No comments:

Post a Comment