Waziri
Mkuu, Kassim Majaliwa akimpongeza Mwenyekiti wa CHADEMA wa kata ya Kangwa
wilayani Songwe ,Keneth Nzowa ambaye pamoja na wenzake walitangaza kukihama
Chama hicho na kujiunga na CCM katika mkutano wa hadhara uliohutubiwa na Waziri
Mkuu kwenye uwanja wa michezo wa Mkwajuni wilayani Songwe Julai 20, 2017.
Waziri
Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Chief Mwibongo wa Ivungu baada ya
kuhutubia mkutano wa hadhara katika uwanja wa michezo wa Mkwajuni wilayani
Songwe Julai 20, 2017. (PICHA NA OFISI
YA WAZIRI MKUU)
NA OWM, SONGWE
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amewahakikishia wananchi kwamba
ahadi zote zilizotolewa na Rais Dkt. John Magufuli katika maeneo mbalimbali
nchini zitatekelezwa, hivyo amewaomba waendelee kuiamini na kushirikiana na Serikali
yao.
Ametoa kauli hiyo jana jioni (Alhamisi, Julai 20, 2017) wakati
akizungumza na wananchi wa wilaya ya Songwe kwenye mkutano wa hadhara
uliofanyika katika uwanja wa Mkuwajuni.Waziri Mkuu yuko Mkoani Songwe kwa ziara
ya kikazi.
Waziri Mkuu alisema kwamba Serikali ya awamu ya Tano ipo makini
na imejipanga vizuri katika kutekeleza ahadi mbalimbali zilizotolewa na Rais
Dkt. Magufuli kama Ilani ya uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka
2015-2020 inavyoelekeza.
Waziri Mkuu aliyasema hayo baada ya mbunge wa jimbo la Songwe,
Mheshimiwa Philipo Mulugo kumuomba awasaidie kumkumbusha Rais Dkt. Magufuli
kuhusu ahadi yake ya ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa kilomita nne
wilayani Songwe.
“Ahadi zote zilizotolewa na Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli
tutazitekeleza, ikiwemo na hii aliyoikumbusha Mheshimiwa Mulugo ya ujenzi wa
kilomita nne za barabara ya lami. Tunawaomba wananchi muendelee kuwa na imani
na Serikali yenu.”
Pia Waziri Mkuu alipiga marufuku wananchi kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya mita
60 kutoka katika vyanzo vya maji na kuwataka washirikiane katika utunzaji wa
mazingira ili kuliepusha Taifa kugeuka jangwa.
Alisema ni vema wananchi wakazingatia Sheria ya Mazingira
inayozuia kufanya shughuli za kibinadamu zikiwemo za kilimo kwenye maeneo yote
ya vyanzo vya maji ndani ya mita 60. Aliwaagiza Wakuu wa Idara kusimamia jambo
hilo.
Waziri Mkuu alisema kwa sasa maeneo mengi yanakabiliwa na
changamoto ya upatikanaji wa maji jambo ambalo linachangiwa na vitendo vya
uharibifu wa mazingira vinavyofanywa na baadhi ya wananchi, hivyo aliwataka
wabadilike.
Hata hivyo, alisema Serikali inaendelea na utekelezaji wa
Kampeni ya Rais Dkt. Magufuli ya kumtua mama ndoo kichwani, ambapo itahakikisha
kwamba wananchi wote wanapata huduma ya maji katika umbali usiozidi mita 400
kutoka kwenye makazi yao.
Pia Waziri Mkuu aliwaeleza wananchi hao
kwamba, Serikali bado inaendelea kutafuta vyanzo mbalimbali vya maji na
kuhakikisha vinabainishwa na kufanyiwa tathmini ili viweze kuendelezwa na
kuongeza upatikanaji wa maji nchini.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Bi. Chiku Gallawa
akizungumzia hali ya upatikanaji wa maji katika mkoa huo alisema watu wanaopata
huduma za maji safi na salama katika maeneo ya mijini ni asilimia 42 na
vijijini ni asilimia 41.6.
Alisema katika bajeti ya 2017/2018 halmashauri za mkoa huo zimetengewa
jumla ya sh bilioni 7.5 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji
ikiwa ni pamoja na ujenzi wa matanki ya kuvunia maji ya mvua katika majengo
yaTaasisi za Umma.
Pia mkoa huo unatekeleza mpango kazi wa usambazaji maji katika
maeneo ya mijini na vijijini kwa kupanua mifumo ya usambazaji na kuzijengea
uwezo mamlaka za maji na ifikapo Desemba mwaka huu wataongeza idadi ya wananchi
wanaopata huduma hiyo kutoka asilimia 45.04 hadi asilimia 55.63.
No comments:
Post a Comment